Thursday, April 16, 2015
Katika moja ya kipindi  cha luninga niliona mabishano baina ya watu watatu, hawa jamaa walitofautiana katika misamiati miwili. Msamiati wa kwanza ni ‘utajiri’ na msamiati wa pili  ni ‘tajiri’. Mmoja alisisitiza ''utajiri ni kuwa na chakula kingi,nguo nyingi na nyumba nyingi'' Wapili alikanusha usemi wa mtu wa kwanza na kaka wa tatu akadakia kwa mbwembwe zote akisema''tajiri au utajiri ni kuwa na kile unachotaka''. Mimi kama mtazamaji nilivutiwa  sana na hayo mazungumzo kiasi cha kuweza kutofautisha hiyo nomino (tajiri) na kivumishi (utajiri) kwa upana. Na kabla msomaji hujafika mbali  naomba kwanza tuelewane katika haya mambo mawili; utajiri na tajiri. Nikisema utajiri namaanisha ni kiasi ama hali ya kuwa na uhuru wa fedha unaoambatana na kumiliki mali na raslimali kwa kiwango  ambacho ni tofauti na watu wengi wanaokuzunguka. Na tajiri ni yule mtu ambaye kafikia hiyo hali ya kumiliki  ukwasi (pesa,mali,raslimali) zaidi , kufuatia mipango, jitihada, malengo na bidii katika uwekezaji alioanza  muda mrefu . Huu mchakato wa muda mrefu unaeleza wazi  kuwa, miongoni mwa matajiri wengi   mafanikio  sio lelemama bali ni jasho itokanayo na kudhibiti  matumizi zidi ya mapato. Kitendo kinachowapelekea  mabilionea  wengi wabakiwe na akiba ambayo hutumika mara mbili. Kwanza katika kununua ‘asset’ na pili kulinda biashara zao.Matumizi ya fedha ya ziada katika kununua assets kama  viwanja, mashamba, nyumba za kupangisha hutoa faida nyingine . Hivyo kunakuwa na utajiri mpya unaoletwa na hizo ‘assets’  .  Mchezo ambao ni mwendelezo kama  vile kuku awezavyo kutotoa mayai na mayai yakaleta kuku wengi zaidi.Na tumizi la pili ni jinsi akiba inavoweza kulinda hazina ya mtu mwenye pesa, kwani  akiba inayotokana na miradi ya tajiri huifadhiwa kwa minajili ya kuokoa jahazi pale tu mambo yanapokwenda mrama.Endapo ikitokea ujasiliamali wa  bilionea  unakumbwa na dhoruba ya madeni na hasara, hadi kuyumbisha mradi. Akiba ya tajiri huyo huja kama nanga inayoweza kulinda mradi wake zidi ya dhoruba (madeni, hasara). Na hivyo kuendelea salama akiwa kifua mbele daima. Mpaka hatua hii bado hatujaona siri kubwa za matajiri, ungependa kuzijua ??,Basi msikilize Bill Gate, Michael Jordan, Steve Jobs, Oprah Winfrey na wengine  wakidadavua siri nane za matajiri.

1. ''Kuzaliwa masikini sio kosa lako,kufa masikini ni kosa''Anatoa siri hiyo  Bill Gate ambaye aliacha chuo na kuonekana hafai hadi pale  alipopigana na kujipatia mafanikio  ya utajiri mkubwa ulioletwa na jitihada ya kuanzisha kampuni yake maarufu duniani kama Microsoft.


2.''Nakubali kuna kushindwa , kila mmoja hushwindwa  ila sikubali  kutojaribu tena' Ni siri ya pili anayotoa Michael Jordan, ambaye amewahi kukataliwa na timu yake ya shule ikisemekana hakuwa na kiwango cha kuridhisha katika mchezo wa kikapu simanzi iliyomfanya kumwaga kilio cha uchungu kama mtoto mchanga . Na leo hii baada ya kutoghairi na'kujaribu tena ' Jordan anaitwa mchezaji bora duniani wa ‘basket’ na mwanamichezo tajiri ulimwenguni.


3.''Kila mmoja ni balozi wa maisha yake , hakuna mwingine atawakilisha au kuishi kwa ajili yako''Ni siri ya tatu anayosema  Oprah Winfey aliyewahi kutimuliwa  kazi katika kituo kimoja cha television kwa madai kuwa hakufiti katika hiyo tasinia ya habari. Jambo lililomfanya ajisimamie na kuwa  vyote ‘balozi’na ‘mtendaji’ wa maisha yake akanzisha kipindi  cha televisheni (oprah show) ambacho kilijichukulia umaarufu mkubwa hata kumfanya afungue kituo binafsi cha tv, Oprah tv network. Uwekezaji uliofungua daraja la ujasiliamali na Oprah kuwa miongoni mwa wanawake matajiri duniani.


4.''Maranyingine unapofanya ubunifu ni rahisi kutenda makosa, ni vyema kuyabaini  mapema (makosa) na kusahihisha'' Hii ni siri ya nne iliyobeba mafanikio ya Steve Jobs, muasisi aliyewahi kusimamishwa kwenye kampuni aliyoianzisha mwenyewe kwa madai ya kutofanya vizuri katika kampuni. Kitendo kilichomfanya aionyeshe dunia yeye ni nani hasa pale linapokuja swala la ubunifu wa  teknolojia'innovation'. Kwani hasira za bwana Steve zimesababisha Ipod na iphone kuheshimika sokoni na yeye kurudi kwenye kampuni yake ya Apple kama kinara wa ubunifi aliyeingia kwenye chati ya matajiri wakubwa duniani.


5''Usiogope kufa,ogopa kutojaribu'' Ni maneno ya bwana Shawn Corey Carter maarufu kama Jay Z. Ambaye alitemwa na kampuni kadhaa zinazojihusisha na usambazaji wa ‘albam’.Kisa kilichomchochea mwanamziku huyo wa miondoko ya kufoka foka kuuza na kusambaza kazi zake mwenyewe . Huku akiwa ni mtoto aliyekuzwa na mzazi mmoja (mama). Jay z hakusita kujaribu .kwa kuuza nakala za kazi yake ndani ya gari dogo, na kwa miguu hadi akajulikana na kupata kianzio. Hatua iliyomfanya awe na njozi njema ya kutengeneza Recording Rebel, mavazi  na uwekezaji kibao hadi kuwa miongoni mwa wasanii tajiri duniani 

.
6.''Siri yangu kuwa  na  biashara iliyofanikiwa ni matokeo ya kujituma kwa   bidii'' Anasema Aliko Dangote ambaye alitoka nyumbani na kwenda kuchapa kazi kwa mjomba wake , mtu muhimu  aliyemsaidia Dangote kupata mtaji na kufanya biashara  za sukari, cement ,.Akawa sio tu muuzaji bali mzalishaji wa hizo bidhaa. Baraka hiyo ni jambo lililofungua njia ya mwafrika huyu kuitwa tajiri wa kwanza Nigeria, Tajiri mkubwa Afrika na tajiri wa kwanza duniani kwa watu  weusi. (kwa muujibu wa gazeti la uchumi, Forbes 2014)


7.''Nafasi ya kuishi ni moja lakini hiyo moja ukiitumia vizuri inatosha'' Ni siri ya saba inayosemwa na kundi la the Beatles ambalo linaundwa na waingereza wanne waliofukuzwa studio kwa kile kinachosemakana' wana sauti mbaya na wasingekuwa na manufaa yeyote katika soko la muziki'. Maneno hayo yaliwafanya The beatles watafute studio zaidi na kupiga kazi kama vichaa hadi kuvunja rekodi ya mauzo hapo Uingereza na Marekani. Baadae  album yao ikaitwa ya kwanza na bora duniani . Hivyo ikawa ni fursa ya kupata pesa na kuwekeza . Nafasi iliyopelekea kupata heshima ya ulimwengu kama kundi bora la muda wote katika miondoko ya ‘rock’ na watu waliokamata fedha chafu zaidi miongoni mwa makundi ya miaka ya 1960.



8.''Mafanikio ni asilimia 1 inayotokana na asilimia 99 ya  kushindwa'' ni siri ya mwisho inayoletwa kwenu  na bwn Soichiro Honda ambaye ni enjinia wa kijapani aliepigwa chini na kampuni ya Toyota baada ya kutomzania kama injinia bora.Soichiro hakuwa na  vigezo ikiwemo elimu ya juu.Na hili hakukubali liwe ndio tatizo, kwani kama wenzake tuliowaona,Soichiro Honda aliendelea kutengeneza mashine za magari na pikipiki huku hatua hiyo ikitafsiriwa na baadhi ya watu kama ni ukanjanja na kushindwa.Mazingira yaliomjengea kiu ya kutaka kufanikiwa haraka.Kabla ya kupata tuzo kutoka ujerumani na kuwa raisi wa kampuni yake mwenyewe inayojulikana kama  Honda Motor Company.Inayofanya vizuri dunia nzima  ,kwa kuzarishi sio tu  piki piki bali pia jenereta,magari,mashine za kufyeka nyasi n,k.

Popular Posts