Saturday, November 8, 2014
Safari ya miguu 100 huanza na hatua moja. Ni kanuni  iliyodarizi safari nyingi za mafanikio. Kutana na safari ya aina hii  inayomhusu mwanafunzi Ben, anayetokea  familia  ya chini yenye mzazi mmoja, anayemudu milo mitatu kwa taabu. Ili watoto wa familia hii  washibe mama anapaswa kujinyima, akihangaika na kazi mbili , tatu au zaidi. Wakati wazazi wengine wameketi na kazi moja  inayowalipa vyema  , mama Ben hukatisha usingizi mnono ili kuanza mapema kazi   za kupiga deki, pasi, kufua  nguo, kuosha vyombo n.k . Mama huyu  huzunguka nyumba  za madokta, maprofesa na watu wengine wenye kipato cha juu ambako hufanya  kazi hizo za ndani . Hali inayomfanya kukimu familia  tu na  asifikirie kuponda raha ama kula bata wasemavyo vijana wa sasa. Hivyo hiyo fedha kidogo anyoipata hugharamia mlo, mavazi na elimu ya wanaye . Kwa hii nafasi mzazi huyu katimiza malengo mawili ; kumkabidhi elimu mtoto wake, na  yeye mwenyewe kumkabidhi mungu naisha yake. Kama kipepeo afuatavyo ua , mmea ufuatavyo jua  .Mwanae Ben anafuatilia elimu kwa umakini mkubwa.Lakini jitihada zinagonga mwamba baada ya kushika nafasi za mwisho darasani. Kitu kinachoibua chachu ya kujaribu tena kwanI Ben anajua fika hana urithi mwingine zaidi ya elimu. Na huo ndio unakua mwanzao wa Ben kukamata nafasi za  kwanza darasani, anafaulu kuingia chuo,na kuchukua masomo ya kitabibu. Hadi leo Ben ni Miongoni mwa madaktari bingwa anayefanya upasuaji wa   ubongo, ikulu ya ufahamu wa binadamu. Dr Ben Carson kafungua taasis ya kusaidia watu wasiojiweza maalufu kama Dr Ben Carson Foundation, kafanya upasuaji mgumu  wa kutenganisha mapacha walioungana vichwa , Dr Ben kapokea tunzo nyingi za heshima na ni muamerika muafrika wa kwanza  kufanya kazi katika kitengo nyeti  cha afya  kilichipo nchini Marekani akiwa na umri mdogo zaidi. Ben sasa ni baba na anafamilia anayoitunza na kuipenda  na sasa ana kula mlo  bora wa chakula cha aina yeyote anachotaka..Mpaka kufika hapo Ben anaorodhesha mambo sita yaliomfanya avune pakacha kubwa la mafanikio kiasi hicho.

1.Kutambua Kipaji. Kila mmoja ana uwezo wa asili katika  kazi,wajibu ama jambo fulani linalohitaji nguvu na akili. Mmoja huweza kuimba,mwinginekuongea, kuongoza,kufundisha n.k ,mmoja kufikiri,mwingine kutenda,kuhamasisha, kushawishi n.k. Huu uwezo binafsi(Kipaji) ukitambulika na kuendelezwa katika nyanja sahihi . Maisha ya kila mmoja wetu yatakuwa bora zaidi.katika Ualimu,uongozi,biashara,sheria,udaktari na kazi nyingine aipendayo.


2.Kuwa muaminifu.Ben,anaona uaminifu kama rangi inayo mtambulisha kila mmoja wetu zidi ya watu wamzungukao.Ukienda kinyume na kuwa raghai watu watakufahamu kwa  tabia hiyo ambayo madhara yake ni kujifungia milango mingi ya fursa zilizo mbele yako.Ila kwa kubakia muaminifu upendo wa jamii,familia na marafiki utaongezeka hata upatikanaji wa nafasi mbalimbali utaongezeka pia, kwa maana uaminifu hujenga  imani na matumaini mioyoni mwa watu wakuzungukao.



3.Jifunze kwa waliofanikiwa.Karibu kila ndoto tulizonazo kuna watu walizitimiza, hivyo ni vyema kujifunza kutokana na hao waliotutangulia kwa kuangalia walianza lini, waliweza vipi, kwa nini walishindwa na kutokata tamaa hata baada ya matatizo kuwa kabili..Kama una ndoto ya uongozi kuna viongozi bora duniani,nchini na mikoani.Kama ni ujasiliamali wapo wa kimataifa,kitaifa,wilaya hadi mtaani.Ukitaka kuwa hodari jifunze kwa mahodari ,na ukitaka kuwa mzuri jifunze toka kwa wazuri.


4.Kuongeza Elimu na maarifa. Unapokuwa na ujuzi, uelewa, na uzoefu lazima uhitajike na kuthaminika Elimu hiyo uliojifunza toka kizazi fulani, shule fulani, darasa fulani, mtaa fulani ina stahili kuongezwa mara kwa mara ili kupata ufanisi mkubwa.Hata kisu kitumikapo bila kunolewa hupoteza makali. . Kadri unavyokuwa na elimu zaidi ndo utakavyokuwa muhimu na wa thamani zaidi.


5.Kutumia Vitabu. Siri za maarifa makubwa zimefichwa katika vitabu vidogo.Utulivu wa fikra za wasomi zipo vitabuni. Mawazo endelevu ya wajuzi walio na busara yapo vitabuni. Hekima ya maelekezo rahisi juu ya mambo magumu  huhifadhiwa katika kurasa za vitabu.Kwa muujibu wa Carson,  usomaji wa maandishi kama vitabu ni maradufu kwa kujenga akili, maarifa na elimu katika kichwa zaidi ya kutazama tv au kusikiliza sauti. 




6.Kuwa na hofu ya mungu. Ben,anaamini kuwa hakuna kipaji,uaminifu, elimu, kujifunza, wala vitabu kama hukumtanguliza mungu mbele. Kwani kila kitu alichoumbiwa mwanadamu kililetwa mbele yake na mungu. Hivyo ni vyema kumuomba mungu akutangulie katika kila jambo unalofanya,na unalotarajia kufanya kwa maana yeye ndio mwenye utaratibu na ratiba ya hatma zetu.






Popular Posts