Thursday, April 16, 2015
Katika moja ya kipindi  cha luninga niliona mabishano baina ya watu watatu, hawa jamaa walitofautiana katika misamiati miwili. Msamiati wa kwanza ni ‘utajiri’ na msamiati wa pili  ni ‘tajiri’. Mmoja alisisitiza ''utajiri ni kuwa na chakula kingi,nguo nyingi na nyumba nyingi'' Wapili alikanusha usemi wa mtu wa kwanza na kaka wa tatu akadakia kwa mbwembwe zote akisema''tajiri au utajiri ni kuwa na kile unachotaka''. Mimi kama mtazamaji nilivutiwa  sana na hayo mazungumzo kiasi cha kuweza kutofautisha hiyo nomino (tajiri) na kivumishi (utajiri) kwa upana. Na kabla msomaji hujafika mbali  naomba kwanza tuelewane katika haya mambo mawili; utajiri na tajiri. Nikisema utajiri namaanisha ni kiasi ama hali ya kuwa na uhuru wa fedha unaoambatana na kumiliki mali na raslimali kwa kiwango  ambacho ni tofauti na watu wengi wanaokuzunguka. Na tajiri ni yule mtu ambaye kafikia hiyo hali ya kumiliki  ukwasi (pesa,mali,raslimali) zaidi , kufuatia mipango, jitihada, malengo na bidii katika uwekezaji alioanza  muda mrefu . Huu mchakato wa muda mrefu unaeleza wazi  kuwa, miongoni mwa matajiri wengi   mafanikio  sio lelemama bali ni jasho itokanayo na kudhibiti  matumizi zidi ya mapato. Kitendo kinachowapelekea  mabilionea  wengi wabakiwe na akiba ambayo hutumika mara mbili. Kwanza katika kununua ‘asset’ na pili kulinda biashara zao.Matumizi ya fedha ya ziada katika kununua assets kama  viwanja, mashamba, nyumba za kupangisha hutoa faida nyingine . Hivyo kunakuwa na utajiri mpya unaoletwa na hizo ‘assets’  .  Mchezo ambao ni mwendelezo kama  vile kuku awezavyo kutotoa mayai na mayai yakaleta kuku wengi zaidi.Na tumizi la pili ni jinsi akiba inavoweza kulinda hazina ya mtu mwenye pesa, kwani  akiba inayotokana na miradi ya tajiri huifadhiwa kwa minajili ya kuokoa jahazi pale tu mambo yanapokwenda mrama.Endapo ikitokea ujasiliamali wa  bilionea  unakumbwa na dhoruba ya madeni na hasara, hadi kuyumbisha mradi. Akiba ya tajiri huyo huja kama nanga inayoweza kulinda mradi wake zidi ya dhoruba (madeni, hasara). Na hivyo kuendelea salama akiwa kifua mbele daima. Mpaka hatua hii bado hatujaona siri kubwa za matajiri, ungependa kuzijua ??,Basi msikilize Bill Gate, Michael Jordan, Steve Jobs, Oprah Winfrey na wengine  wakidadavua siri nane za matajiri.

1. ''Kuzaliwa masikini sio kosa lako,kufa masikini ni kosa''Anatoa siri hiyo  Bill Gate ambaye aliacha chuo na kuonekana hafai hadi pale  alipopigana na kujipatia mafanikio  ya utajiri mkubwa ulioletwa na jitihada ya kuanzisha kampuni yake maarufu duniani kama Microsoft.


2.''Nakubali kuna kushindwa , kila mmoja hushwindwa  ila sikubali  kutojaribu tena' Ni siri ya pili anayotoa Michael Jordan, ambaye amewahi kukataliwa na timu yake ya shule ikisemekana hakuwa na kiwango cha kuridhisha katika mchezo wa kikapu simanzi iliyomfanya kumwaga kilio cha uchungu kama mtoto mchanga . Na leo hii baada ya kutoghairi na'kujaribu tena ' Jordan anaitwa mchezaji bora duniani wa ‘basket’ na mwanamichezo tajiri ulimwenguni.


3.''Kila mmoja ni balozi wa maisha yake , hakuna mwingine atawakilisha au kuishi kwa ajili yako''Ni siri ya tatu anayosema  Oprah Winfey aliyewahi kutimuliwa  kazi katika kituo kimoja cha television kwa madai kuwa hakufiti katika hiyo tasinia ya habari. Jambo lililomfanya ajisimamie na kuwa  vyote ‘balozi’na ‘mtendaji’ wa maisha yake akanzisha kipindi  cha televisheni (oprah show) ambacho kilijichukulia umaarufu mkubwa hata kumfanya afungue kituo binafsi cha tv, Oprah tv network. Uwekezaji uliofungua daraja la ujasiliamali na Oprah kuwa miongoni mwa wanawake matajiri duniani.


4.''Maranyingine unapofanya ubunifu ni rahisi kutenda makosa, ni vyema kuyabaini  mapema (makosa) na kusahihisha'' Hii ni siri ya nne iliyobeba mafanikio ya Steve Jobs, muasisi aliyewahi kusimamishwa kwenye kampuni aliyoianzisha mwenyewe kwa madai ya kutofanya vizuri katika kampuni. Kitendo kilichomfanya aionyeshe dunia yeye ni nani hasa pale linapokuja swala la ubunifu wa  teknolojia'innovation'. Kwani hasira za bwana Steve zimesababisha Ipod na iphone kuheshimika sokoni na yeye kurudi kwenye kampuni yake ya Apple kama kinara wa ubunifi aliyeingia kwenye chati ya matajiri wakubwa duniani.


5''Usiogope kufa,ogopa kutojaribu'' Ni maneno ya bwana Shawn Corey Carter maarufu kama Jay Z. Ambaye alitemwa na kampuni kadhaa zinazojihusisha na usambazaji wa ‘albam’.Kisa kilichomchochea mwanamziku huyo wa miondoko ya kufoka foka kuuza na kusambaza kazi zake mwenyewe . Huku akiwa ni mtoto aliyekuzwa na mzazi mmoja (mama). Jay z hakusita kujaribu .kwa kuuza nakala za kazi yake ndani ya gari dogo, na kwa miguu hadi akajulikana na kupata kianzio. Hatua iliyomfanya awe na njozi njema ya kutengeneza Recording Rebel, mavazi  na uwekezaji kibao hadi kuwa miongoni mwa wasanii tajiri duniani 

.
6.''Siri yangu kuwa  na  biashara iliyofanikiwa ni matokeo ya kujituma kwa   bidii'' Anasema Aliko Dangote ambaye alitoka nyumbani na kwenda kuchapa kazi kwa mjomba wake , mtu muhimu  aliyemsaidia Dangote kupata mtaji na kufanya biashara  za sukari, cement ,.Akawa sio tu muuzaji bali mzalishaji wa hizo bidhaa. Baraka hiyo ni jambo lililofungua njia ya mwafrika huyu kuitwa tajiri wa kwanza Nigeria, Tajiri mkubwa Afrika na tajiri wa kwanza duniani kwa watu  weusi. (kwa muujibu wa gazeti la uchumi, Forbes 2014)


7.''Nafasi ya kuishi ni moja lakini hiyo moja ukiitumia vizuri inatosha'' Ni siri ya saba inayosemwa na kundi la the Beatles ambalo linaundwa na waingereza wanne waliofukuzwa studio kwa kile kinachosemakana' wana sauti mbaya na wasingekuwa na manufaa yeyote katika soko la muziki'. Maneno hayo yaliwafanya The beatles watafute studio zaidi na kupiga kazi kama vichaa hadi kuvunja rekodi ya mauzo hapo Uingereza na Marekani. Baadae  album yao ikaitwa ya kwanza na bora duniani . Hivyo ikawa ni fursa ya kupata pesa na kuwekeza . Nafasi iliyopelekea kupata heshima ya ulimwengu kama kundi bora la muda wote katika miondoko ya ‘rock’ na watu waliokamata fedha chafu zaidi miongoni mwa makundi ya miaka ya 1960.



8.''Mafanikio ni asilimia 1 inayotokana na asilimia 99 ya  kushindwa'' ni siri ya mwisho inayoletwa kwenu  na bwn Soichiro Honda ambaye ni enjinia wa kijapani aliepigwa chini na kampuni ya Toyota baada ya kutomzania kama injinia bora.Soichiro hakuwa na  vigezo ikiwemo elimu ya juu.Na hili hakukubali liwe ndio tatizo, kwani kama wenzake tuliowaona,Soichiro Honda aliendelea kutengeneza mashine za magari na pikipiki huku hatua hiyo ikitafsiriwa na baadhi ya watu kama ni ukanjanja na kushindwa.Mazingira yaliomjengea kiu ya kutaka kufanikiwa haraka.Kabla ya kupata tuzo kutoka ujerumani na kuwa raisi wa kampuni yake mwenyewe inayojulikana kama  Honda Motor Company.Inayofanya vizuri dunia nzima  ,kwa kuzarishi sio tu  piki piki bali pia jenereta,magari,mashine za kufyeka nyasi n,k.

Friday, March 20, 2015

Binafsi nimezoe miradi ya familia ni maduka ya bidhaa kama simu, nguo, mifugo, daladala, n.k. Ambayo huanza na kasi ,baadae kudorora na baadhi ya miradi kupotea kabisa.Tafiti zinaonyesha kuwa kati ya  miradi mitatu ya familia ni mradi mmoja tu hudumu.Na kwa huo mradi unaodumu hakika uongozi  ni sindano kubwa katika kufuma timu ya usimamizi wake.Wakati biashara hii inayomilikiwa kiasi kikubwa na wanafamilia inategemea sana menegementi bora. Mataifa ya Izrael , Canada ambayo uchumi wake umestawishwa kwa zaidi ya asilimia 65 na miradi ya familia.Wanatambua siri nyingine za kufanikiwa kwa biashara zao. Moja, ni mgawanyo wa majaukumu baina ya wanafamilia. Baba, mama ,kaka  na dada anahusika na jukumu moja moja kati ya uhasibu, matangazo, utafiti, soko na maboresho. Korea na India ambao pia ni majabari wa miradi ya familia. Wanatambua fika kuwa,ukuu wao katika hizo biashara ni matokeo mazuri ya kuweka mipango ya kudumu ambayo hufuatwa na kila kizazi kinachorisishwa mradi. Palestine taifa lenye miradi mingi ya famillia kama kitovu cha uchumi wake, pia wanang’oa mizizi ya maendeleo yao. Wakibainisha kuwa kutoweka hisia za ndani katika hizi biashara ni nyota njema inayoangaza mafanikio ya miradi ya familia.Katika suala la hisia mtama zaidi unamwagwa  kuwa,sio kila ndugu ajiriwe au kupata huduma ya bure, ila vigezo na masharti vizingatiwe. Na Italy ambao ni watengenezaji suti wazuri wameachia mikono ya familia inue haya mavazi ya thamani  katika kila  jicho la ulimwengu. Zaidi ya asilimia 90  ya miradi ya kifamilia nchini humo huepuka matumizi mabaya ya faida inayozalishwa na mradi , jambo linalozuia mparaganyiko na kusambaratika kwa biashara zao.Ikumbukwe tu kuwa miradi hii ni ya aina nyingi kama vidonge.Kuna miradi mikubwa kuna miradi midogo.Barafu,karanga,na nyanya za magengeni ni miradi ya familia yenye sura ndogo.Makampuni ya gari,simu,vitabu , ni  miradi ya familia yenye sura kubwa.Unafahamu biashara kubwa za kifamilia ambazo zitakuacha mdomo wazi ?,Basi usichoke, tazama namba moja hadi kumi hapa chini.
1.Toyota

2.Ford Motor

3.Tata group

4.Volkswagen

5.Samsung

6.LG

7.Motorola

8.Siemens

9.Kodak

10.World Wrestling Entertainment(WWE)



Friday, February 27, 2015
Wakati sauti  hujaribu kudokeza baadhi ya tabia za ndani, mavazi   hodokeza mawazo, fikra na hisia za mtu .Hii hutokana  na muonekano  unaoletwa na uteuzi wa nguo ambazo huwa na rangi mbalimbali.Mfano katika shule sio jambo geni mwanafunzi kumtambua mwalimu aliye na hasira , kwa kutumia aina ya nguo  alizovaa. Hata katika usafiri ni rihasi kubaini hadhi ya mtu kwa kutumia nguo tu .Kwa maana mavazi ni lugha ya ishara inayojisimamia bila sauti. Nakumbuka siku moja nikiwa jijini mwanza ,katika moja ya kituo  cha magari madogo maarufu kama daladala.Nilishuudia kijana  akikosa msaada ilihali alikuwa na shida kubwa. Kijana alielekea kwa mzee kuomba msaada wa nauli.Mzee  ni baba wa makamo kwa sauti na jicho alivyomkazia muomba msaada.Kinyume  na fikira zangu ,yule mzee hakutoa hata shilingi .Baaadala yake  akadai asingeweza kumpatia kijana fedha.kwani kijana alikuwa na maisha mazuri. Dhana iliyoletwa na  kijana kuvaa kofia nyekundi, shati jeusi , kaptula jekundu , soksi nyeusi viatu vyekundu na kitambaa cheusi. Mwisho jitihada zilivyogonga mwamba, kijana akatoweka' kilaini' kama wasemavyo waswahili wa kisasa.Tukio hili  halipo mbali na wasemavyo wanasaikolojia, wataalamu wa tabia,akili na mienendo  ya binadamu.Ambao wamethibitisha kuwa  tamaduni na mazingira mbalimbali ni sababu kuu zinzopelekea mavazi kupewa maana tofauti tofauti katika jamii.Wakielezea kwa undani zaidi,wataalam hao wanadai mavazi ya rangi ,nyekundu, blue, nyeupe, nyeusi, njano na kijani yana maana zifuatazo.

1.Nguo za rangi nyekundu.ni mavazi yanaofananishwa na taswira ya damu au moto.Kwa baadhi ya watu huwa ni vazi linalomaanisha nguvu,mabavu na utawala ,jambo linalopelekea mtu huyu kupewa umakini katika kundi la watu.Pia vazi jekundu ni ishara ya upendo wa dhati kama linavyopewa umuhimu katika harusi za kihindi,kijapani na vipindi vya valentine day pamoja na Christmas.Lakini pia kwa baadhi ya tamaduni, vazi jekundu hutafsiriwa kama kiashiria cha hatari au vita


2.Nguo za rangi ya Blue mara nyingi huwakilisha bahari na anga.Hii  ranga kupendwa na wanaume zaidi.Mtu mwenye sharti, t shirt au vazi lolote la blu,hutafsriwa na jamii kama tu  muaminifu,mkweli,mpole ,mwenye kujiamini na mtulivu.Lakini pia kuna mazingira mengine ambayo huashiria vazi la blue kama huzuni


3.Nguo za rangi ya kijani.Wakati hii rangi husadifu uoto wa asili,kijani kibichi na mazingira.Vazi la kijani hutambulisha mtu kama anayekuaa,anayebadilika na kujitegemea .Kwa miaka mingi  kijani imekuwa ni rangi inayohusishwa na maswala ya uchumi pamoja na fedha.


4.Nguo za rangi Nyeupe.Hii rangi huchukuliwa kama taswira ya nuru au mwanga hivyo hata kufanya mavazi meupe kuonyesha watu wanaoweza kuleta matumaini,kama madaktari. Pia huashiria usafi, utimilifu uungwana na mtu asiye na hatia.Kama walivyo baadhi ya mabibi harusi ndani ya shela,na  viongozi wa dini ndani ya kanzu na majoho meupe

5.Nguo za rangi ya Manjano(njano).Hii ni rangi inayojumuisha mchanganyiko wa nyekundu na nyeupe kama wakati wa mawio au jua la asubuhi.Njano ikiwa ni miongoni mwa rangi ing'aayo sana,Vazi lake  humaniisha mvaaji ana furaha, ni tegemezi, mshindi, mtaka uhuru.Nchini Japani na china manjano ni rangi ya watu wenye hadhi ya juu na kueshimika.

6.Nguo za rangi nyeusi ni kielelezo cha upotevu wa rangi nyingine na mtu aliye vaa shati ,suruali au gauni nyeusi inaatafsiriwa ana huzuni au majonzi(utamaduni wa kimagharibi),,Pia kwa baadhi ya mazingira vazi jeusi huwa ni ishara ya usiriasi,mamlaka,na ukuu.Kama zilivyo maarufu suti nyeusi,na viongozi wa serikali. kadharika joho jeusi na mahakimu

Monday, December 8, 2014
Kwa muda mwingi wasanii wamekuwa wazungumzaji wakuu , wakisema visa na mikasa ya kila siku.Sauti zao hujadili makosa ya jamii, mafanikio ya jamii n.k. Wakati wakiongelea  makosa ambayo huambatanishwa na shughuri za kibinadamu zisizofanikiwa au kutekelezwa kwa kiwango stahiki. Pia wasanii huangaza mafanikio ya watu katika jamii kwa kutazama  jitihada za mwanaume au mwanamke zilizotoa matunda katika utaftaji wa maisha bora.Msaani mmoja anapofanikisha kuongea juu ya kushindwa na kufaulu kwa kugusia shida na raha lazima kazi yake ipendwe na jamii.Vile vile msanii anapoweza kutia moyo watu au  mtu aliyepoteza matumaini ya kuishi halikadhalika kazi yake hupendwa.  Na pale huyu msanii akifumbua fumbo  gumu kwa wananchi, mchango wake daima hausahauliki mapema. Katika jopo la la watu ambao ni kioo cha jamii ,hatuwezi kuwasahau wanamuziki. Kwa kuwa ni miongoni mwa wasanii muhimu katika jamii, ambao hugeuka waalimu na kutoa maarifa ya mambo yatukabiliyo kila mara. Hivyo nakusihi ufuatilie kile wasnii wa Afrika mashariki wanachosema   kuhusu maisha.

1.''maisha ni kama safari ni safari hakuna ajuaye kesho itakuaje''Jaquar


2.''Maisha ni sawa na kupiga mbizi,leo juu kesho chini,usinicheke kukosa.''Twanga pepeta.

3''Maisha ya mtaani ninanayo yaona sio sawa na ya shule niliyoyasoma''FID Q,na witness



4.'' Maisha ni fumbo fumbua,maisha ni bahati ,ifumbate  maisha ni mapigano,pigana'' Mwijuma Muumin

5.''Maisha ni kitendawili kigumu sana leo umepata kesho umekosa'' kimobitel

6.''maisha ni tendo lifanikishe,maisha ni huzuni ishinde,maisha ni mtihani faulu'' Mwijuma Muumin

7 .''Maisha ni safari nitafika msafiri kwa imani ya kuamnika sitofichwa kama siri''One the Incredible

8. ''maisha ni karata unaweza ukalamba dume,ukalamba garasha, ukalamba mzungu wa nne''Geez Mabovu



Tuesday, December 2, 2014
Mwezi novemba  mwaka 2014 nilifika mkoa fulani hapa Tanzania kwa ajili ya mahafali . Na kwa kuwa  matumizi ya simu za kisasa''smartphone'' ni makubwa  kwa kila mmoja ili nibidi ninunue simu ya dizaini hiyo ilahisishe mambao yangu. Hii ilikuwa ni simu ya tecno H6 iliyoweza kupiga picha za ubora mzuri kama zile za kamera ya kawaida. Ila mungu si Athumani asubuhi ya keshokutwa, siku mbili baadae,  niliamkia mazoezini kama ada yangu . Nikikimbia kando ya bahari ya hindi kwa muda wa nusu saa hali iliopelekea kuchoka sana kwani ni muda sijafanya joging. Hata jioni nikiwa katika mgahawa mmoja ,najivinjari kwa smartphone mkono wa kushoto na maji mkono wa kulia nikinywa taratibu kwa fundo la kizembe bado nilihisi uchovu wa mwili na akili uliotokana na zoezi la asubuhi. Baadae kidogo niliondoka eneo hilo la chuo kulipokuwa na mgahawa nakuelekea nje. Nikiwa nje nilitaka kuwajuza marafiki zangu kuwa nipo tayari mkoani hapo,  ndio ghafla nashishituka sina simu mfukoni wala mkononi. Japo akili ilikuwa imechoka ,  niliweza kumbuka kuwa , kabla ya kulipia maji kwa muhudumu niliacha simu mezani na sikuichukua wakati naondokka eneo hilo. Nikafanya jitihada za kumdadisi mhudumu hakuweza kufahamu lolote. Nikauliza watu waliokuwa karibu yangu wakitazama mechi ya West Brom na Arsenal Betting iliyochezwa siku hiyo ya jumamosi tarehe 29 novemba , nao pia walikana  kuiona smartphone yangu mpya iliyokuwa na siku tatu tu toka ninunue. Hatimaye nimeuliza mtandaoni na majibu yao yameshauri matumizi ya programm zifuatazo.


1. LOOKOUT. Hii ni moja ya programm inayomwezesha mmliki wa simu aina ya android kubaini mienendo ya simu iliyopotea. Huku ikitoa taarifa  mahala simu ilipo , Pia hii programu inapiga picha za siri bila mwizi au aliyechukua kutambua na kutuma moja kwa moja  kwa  anuani yako uliojisajilia katika hiyo programm.Ina uwezo wa kufunga ama kufuta habari binafsi zilizondani ya simu na endappo upo karibu na mtu mwenye simu yako programm inakuwezesha  kuruhusu simu itoe alarm na kumkamata mwizi.




2. LOOKOUT PLAN B. Tofauti ya programm hii na ya kwanza ni kuwa Lookout plan B hutumika na baadhi ya simu tu zinazotumia mifumo ya android. Na wakati programm zote katika hii list zinahitaji kuwekwa katika simu kabla haijaibiwa, Lookout plan b inaweza kuingizwa katika kifaa kilichopotea ama kuibiwa hata baada ya mwizi kutokomea Ni kwa njia ya mtandao Lookout Plan B huweza kufikia simu iliyopokonywa.



3. PREY. Kama zilivyo programm nyingine hii pia inapatikana Google play , yaani katika simu zitumiazo android . Au kwa urahisi sana zinajulikana kwa jina la '' simu za tachi' '(touch). Prey ni programm ambayo inauwezo wa kuonyesha mitandoo yote inayotumiwa na simu yako iliyopotea. Lakini hata kama kulikuwa na picha za muhimu hii ni prograam iayoweza kuzihifadhi katika account au anuani yako ya google.Zaid Prey huweza kutumika hata kutafta laptop na tablets zilizopotea.





4. FIND MY PHONE. Hii programm inatofautiana na nyingine kwa kuwa inawafaa watumiaji wa Iphone na vifaa vingine vinavyotengenezwa na  kampuni  ya Mac.Ambao ni wazalishaji wa ipod, ipad na simu zaIphone.  Habari nyeti za mtu alizoacha katika simu hupelekwa na  progrmm hii hadi uwanja wa icloud. ambako mmliki wa simu hufika kwa kufanya usajili mdogo. Hapa utajua simu yako iko wapi, nani anaitumia kwa kutazama picha zilizopigwa kwa usiri wakati mwizi akiitumia.
                                                                                     






5. ANDROID DEVICE MANAGER, Ni aina nzuri ya programm katika kurudisha simu kwa kuwa ina sifa kama programm nyingine ikiwemo ile ya kuwafaa watumiaji wa android, Pia ina mambo muhimu ya kuzingatia kama ; kupata simu iliyopotea .kwanza. inatakiwa iwe imeunganishwa na mtandao, pili,  iunganishwe na na programm hii kabla haijaibiwa,  tatu, simu itaonekana baada ya kuwa karibu na minara ya simu, huduma za wireless, bloothooth na mifumo mingine yenye kutuma mawasiliano katika satellite za google , nne, kuifikia simu iliyopotea unatakiwa kutumia simu tofauti, computer au kifaa kingine. Mwisho hii programm kama hizo zilizotajwa juu hupata simu ikiwa imewashwa na sio kuzimwa

.Kumbuka ni vyema kutoa taarifaya upotevu wa mali yako katika uongozi wa serikali kama polisi au ofisi ya kijiji kabla ya kufanya ufuatiliaji kwa kutumia programm hizi.

Saturday, November 8, 2014
Safari ya miguu 100 huanza na hatua moja. Ni kanuni  iliyodarizi safari nyingi za mafanikio. Kutana na safari ya aina hii  inayomhusu mwanafunzi Ben, anayetokea  familia  ya chini yenye mzazi mmoja, anayemudu milo mitatu kwa taabu. Ili watoto wa familia hii  washibe mama anapaswa kujinyima, akihangaika na kazi mbili , tatu au zaidi. Wakati wazazi wengine wameketi na kazi moja  inayowalipa vyema  , mama Ben hukatisha usingizi mnono ili kuanza mapema kazi   za kupiga deki, pasi, kufua  nguo, kuosha vyombo n.k . Mama huyu  huzunguka nyumba  za madokta, maprofesa na watu wengine wenye kipato cha juu ambako hufanya  kazi hizo za ndani . Hali inayomfanya kukimu familia  tu na  asifikirie kuponda raha ama kula bata wasemavyo vijana wa sasa. Hivyo hiyo fedha kidogo anyoipata hugharamia mlo, mavazi na elimu ya wanaye . Kwa hii nafasi mzazi huyu katimiza malengo mawili ; kumkabidhi elimu mtoto wake, na  yeye mwenyewe kumkabidhi mungu naisha yake. Kama kipepeo afuatavyo ua , mmea ufuatavyo jua  .Mwanae Ben anafuatilia elimu kwa umakini mkubwa.Lakini jitihada zinagonga mwamba baada ya kushika nafasi za mwisho darasani. Kitu kinachoibua chachu ya kujaribu tena kwanI Ben anajua fika hana urithi mwingine zaidi ya elimu. Na huo ndio unakua mwanzao wa Ben kukamata nafasi za  kwanza darasani, anafaulu kuingia chuo,na kuchukua masomo ya kitabibu. Hadi leo Ben ni Miongoni mwa madaktari bingwa anayefanya upasuaji wa   ubongo, ikulu ya ufahamu wa binadamu. Dr Ben Carson kafungua taasis ya kusaidia watu wasiojiweza maalufu kama Dr Ben Carson Foundation, kafanya upasuaji mgumu  wa kutenganisha mapacha walioungana vichwa , Dr Ben kapokea tunzo nyingi za heshima na ni muamerika muafrika wa kwanza  kufanya kazi katika kitengo nyeti  cha afya  kilichipo nchini Marekani akiwa na umri mdogo zaidi. Ben sasa ni baba na anafamilia anayoitunza na kuipenda  na sasa ana kula mlo  bora wa chakula cha aina yeyote anachotaka..Mpaka kufika hapo Ben anaorodhesha mambo sita yaliomfanya avune pakacha kubwa la mafanikio kiasi hicho.

1.Kutambua Kipaji. Kila mmoja ana uwezo wa asili katika  kazi,wajibu ama jambo fulani linalohitaji nguvu na akili. Mmoja huweza kuimba,mwinginekuongea, kuongoza,kufundisha n.k ,mmoja kufikiri,mwingine kutenda,kuhamasisha, kushawishi n.k. Huu uwezo binafsi(Kipaji) ukitambulika na kuendelezwa katika nyanja sahihi . Maisha ya kila mmoja wetu yatakuwa bora zaidi.katika Ualimu,uongozi,biashara,sheria,udaktari na kazi nyingine aipendayo.


2.Kuwa muaminifu.Ben,anaona uaminifu kama rangi inayo mtambulisha kila mmoja wetu zidi ya watu wamzungukao.Ukienda kinyume na kuwa raghai watu watakufahamu kwa  tabia hiyo ambayo madhara yake ni kujifungia milango mingi ya fursa zilizo mbele yako.Ila kwa kubakia muaminifu upendo wa jamii,familia na marafiki utaongezeka hata upatikanaji wa nafasi mbalimbali utaongezeka pia, kwa maana uaminifu hujenga  imani na matumaini mioyoni mwa watu wakuzungukao.



3.Jifunze kwa waliofanikiwa.Karibu kila ndoto tulizonazo kuna watu walizitimiza, hivyo ni vyema kujifunza kutokana na hao waliotutangulia kwa kuangalia walianza lini, waliweza vipi, kwa nini walishindwa na kutokata tamaa hata baada ya matatizo kuwa kabili..Kama una ndoto ya uongozi kuna viongozi bora duniani,nchini na mikoani.Kama ni ujasiliamali wapo wa kimataifa,kitaifa,wilaya hadi mtaani.Ukitaka kuwa hodari jifunze kwa mahodari ,na ukitaka kuwa mzuri jifunze toka kwa wazuri.


4.Kuongeza Elimu na maarifa. Unapokuwa na ujuzi, uelewa, na uzoefu lazima uhitajike na kuthaminika Elimu hiyo uliojifunza toka kizazi fulani, shule fulani, darasa fulani, mtaa fulani ina stahili kuongezwa mara kwa mara ili kupata ufanisi mkubwa.Hata kisu kitumikapo bila kunolewa hupoteza makali. . Kadri unavyokuwa na elimu zaidi ndo utakavyokuwa muhimu na wa thamani zaidi.


5.Kutumia Vitabu. Siri za maarifa makubwa zimefichwa katika vitabu vidogo.Utulivu wa fikra za wasomi zipo vitabuni. Mawazo endelevu ya wajuzi walio na busara yapo vitabuni. Hekima ya maelekezo rahisi juu ya mambo magumu  huhifadhiwa katika kurasa za vitabu.Kwa muujibu wa Carson,  usomaji wa maandishi kama vitabu ni maradufu kwa kujenga akili, maarifa na elimu katika kichwa zaidi ya kutazama tv au kusikiliza sauti. 




6.Kuwa na hofu ya mungu. Ben,anaamini kuwa hakuna kipaji,uaminifu, elimu, kujifunza, wala vitabu kama hukumtanguliza mungu mbele. Kwani kila kitu alichoumbiwa mwanadamu kililetwa mbele yake na mungu. Hivyo ni vyema kumuomba mungu akutangulie katika kila jambo unalofanya,na unalotarajia kufanya kwa maana yeye ndio mwenye utaratibu na ratiba ya hatma zetu.






Popular Posts